Njombe, Iringa Waponda Matokeo Darasa La Saba | MIKENTOBI MIKENTOBI - A Blog with updated posts about events and current issues!
NEWS UPDATE :
Over a 100,000 ways to Earn Online!Sale Online!
Labels :
Home » » Njombe, Iringa Waponda Matokeo Darasa La Saba

Njombe, Iringa Waponda Matokeo Darasa La Saba

Written By Mike Ntobi on Wednesday, December 26, 2012 | 7:25 AM


Na: Shaban Lupimo, Njombe
WANASIASA wa Mikoa ya Iringa na Njombe  wameponda matokeo ya darasa la saba yaliyotangazwa  na Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi Dk Shukuru Kawambwa, kwa kusema kuwa Serikali inapika bomu la wasomi ambao hawatakuwa na tija kwa  taifa.


Wanasiasa hao walitoa kauli hiyo juzi  katika mkutano wa kuchagua wanafunzi watakaojiunga na kidato cha kwanza katika muhula ujao wa masomo wa mwaka 2013 kwa kanda ya Iringa, uliofanyika mjini Njombe ambapo walielezewa kushangazwa kwao na Serikali kuchagua hata wanafunzi wenye ufaulu D kwenda sekondari.

Mbunge wa Jimbo la Iringa mjini, Mchungaji Peter Msigwa (Chadema) alisema elimu ya Tanzania imekosa mwelekeo kutokana na mwaka huu Wizara ya Elimu kuchagua wanafunzi wa kujiunga na kidato cha kwanza mpaka waliopata wastani wa alama ya asilimia 24 kwa kila somo, badala ya asilimia 44 ili kujaza nafasi katika shule za sekondari.

“Serikali inapika bomu la wasomi ambao hawatakuwa na manufaa kwa taifa, kwa sababu haiwezekani kuchagua mpaka mwanafunzi asiyekuwa na sifa ya kujiunga na kidato cha kwanza ili kujaza nafasi, wasomi hawa ndio wale wanaopasua watu vichwa badala ya miguu,” alisema Msigwa.

Mchungaji Msigwa aliitaka Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi kuacha kujitapa kwamba mwaka huu wanafunzi wamefanya vizuri ikilinganishwa na mwaka jana, wakati wamechukua mpaka wale waliofeli kujiunga na elimu ya sekondari na kuitaka Wizara ya  elimu na mafunzo ya Ufundi kueleza sababu ya  kushusha alama za ufaulu kwa  wanafunzi mwaka huu. 

NayeMbunge wa Jimbo la Ludewa, Deo Filikujombe (CCM) alisema haina maana kuona taifa linapeleka wanafunzi wengi sekondari wakati waliofaulu ni wachache.

“Mimi naona haina maana kujisifia kuwa tumefaulisha na kupeleka sekondari wanafunzi wengi wakati waliofaulu wachache, kama wamefaulu wanafunzi 100 tupeleke hao hao badala ya 200 ili kujaza shule,” alisema Filikujombe.

Filikunjombe alipendekeza wanafunzi ambao  wamepata wastani wa alama ya chini ya asilimia 70 kuachwa kabisa kuchaguliwa kujiunga na elimu ya sekondari,  badala ya kuwapeleka sekondari ili kwenda kujaza  vyumba vya madarasa wakati hawana sifa ya kujiunga na elimu hiyo.
Share this article :

Related Posts :

Post a Comment

 
Support : MIKENTOBI | Creating Website | Johny Template | Mas Template | UviOo | SFI

Copyright © 2010 - 2014. MIKENTOBI - All Rights Reserved
Template Created by Creating Website Modified and Published by MIKENTOBI
Proudly powered by Blogger